Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Madaba limeketi leo Januari 30, 2026 katika Ukumbi wa Halmashauri kujadili na kupokea taarifa za utekelezaji wa shughuli za Kamati za Kudumu kwa robo ya pili ya mwaka wa fedha.
Kikao hicho kililenga kufanya tathmini ya utekelezaji wa mipango na miradi ya maendeleo pamoja na hali ya utoaji wa huduma kwa wananchi katika kipindi husika, kwa lengo la kuongeza ufanisi na uwajibikaji katika shughuli za Halmashauri.
Katika kikao hicho, wajumbe wa kamati mbalimbali waliwasilisha taarifa zao na kueleza mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizojitokeza pamoja na mapendekezo ya kuboresha utendaji kazi. Waheshimiwa Madiwani walipata nafasi ya kujadili kwa kina taarifa hizo, kutoa maelekezo na kushauri njia bora za kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya kamati na kuleta matokeo chanya kwa wananchi.
Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Madaba, Mhe. Moses Fwiling’hafu, alisisitiza umuhimu wa kuongeza na kudhibiti mapato ya Halmashauri ili kuondoa mianya ya upotevu wa mapato.
Alitoa maelekezo kwa wataalam kuwa na uangalizi wa karibu katika usimamizi wa vyanzo vya mapato, hususan katika sekta ya kilimo, ardhi, maliasili pamoja na kuhakikisha sheria na taratibu zilizopo zinafuatwa kikamilifu.
Aidha, Mwenyekiti huyo aliwataka watendaji wa kata kuanza kuwatambua wawekezaji wote waliopo katika maeneo yao ili waweze kushirikishwa kikamilifu katika shughuli za maendeleo na kuchangia ustawi wa Halmashauri ya Madaba.
Kikao hicho ni sehemu ya juhudi za Halmashauri kuimarisha uwajibikaji, kusimamia rasilimali za umma na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora kupitia utekelezaji wa miradi na mipango ya maendeleo.
MADABA - RUVUMA
Anwani ya Posta: 38 BARABARA YA KIFAGURO MAGINGO, P.O.BOX 10, 57186 MADABA, SONGEA
Simu: 0252951052
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ded@madabadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Madaba.Haki zote zimeifadhiwa